Sunday, 23 September 2018

MKARIBIE YEHOVA ZAIDI



Kujifunza juu ya Yehova ni hatua muhimu ya kumkaribia. Ni hatua inayopaswa kuendelea daima. Tuseme unaota moto wakati wa usiku wenye baridi, je, ungeuacha moto huo ufifie na kuzimika? Hapana. Utaendelea  kuongeza kuni ili moto uendelee kuwaka. Huenda uhai wako unautegemea! Sawa na vile kuni huchochea moto, ndivyo “kumjua Mungu” kunavyoimarisha upendo wetu kwa Yehova.—Methali 2:1-5.
Mwanamume akiota moto huku akiongeza kuni
Kama moto, Upendo wako kwa Yehova unahitaji kuchochewa ili uendelee kuwaka
11. Mafundisho ya Yesu yalikuwa na matokeo gani kwa wanafunzi wake?
11 Yesu alitaka wanafunzi wake waendelee kuimarisha upendo wao kwa Yehova na Neno lake la kweli lenye thamani. Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wawili baadhi ya unabii ulio katika Maandiko ya Kiebrania ambao ulitimizwa maishani mwake. Matokeo yakawaje? Baadaye walisema hivi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia Maandiko?”—Luka 24:32.
12, 13. (a) Upendo wa watu wengi ulimwenguni kumwelekea Mungu na Biblia ukoje? (b) Tunawezaje kuendeleza upendo wetu?
12 Ulipojifunza kwa mara ya kwanza mambo ambayo Biblia inafundisha hasa, je, hukufurahi sana, ukawa na bidii na upendo mwingi sana kumwelekea Mungu? Bila shaka. Wengi wamehisi hivyo. Kazi kubwa sasa ni kuendelea kukuza na kuimarisha upendo huo. Hatutaki kuuiga ulimwengu. Yesu alitabiri hivi: “Upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Unawezaje kuendelea kumpenda Yehova na kweli zake zilizo katika Biblia?
13 Endelea kupata ujuzi juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Tafakari au fikiria kwa uzito mambo unayojifunza katika Neno la Mungu, na ujiulize: ‘Mambo hayo yananifundisha nini juu ya Yehova Mungu? Yananisaidiaje kumpenda Yehova zaidi kwa moyo, akili, na nafsi yangu yote?’ (1 Timotheo 4:15) Kutafakari juu ya mambo hayo kutakufanya umpende Yehova zaidi.
14. Sala inawezaje kutusaidia kuendelea kukaa katika upendo wa Yehova?
14 Njia nyingine ya kuimarisha upendo wako kwa Yehova ni kusali kwa ukawaida. (1 Wathesalonike 5:17) Katika  Sura ya 17 ya kitabu hiki tulijifunza kwamba sala ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Kama vile uhusiano kati ya wanadamu husitawi kwa sababu ya kuwasiliana kwa uhuru na kwa ukawaida, uhusiano wetu na Yehova hukua na kuimarika tunaposali kwa ukawaida. Hatupaswi kusali kidesturi tu, tukirudia-rudia maneno yaleyale bila hisia wala maana yoyote. Tunapaswa kuzungumza na Yehova kama vile mtoto anavyozungumza na baba anayempenda. Bila shaka, tunataka kuzungumza kwa heshima, lakini waziwazi, kwa unyoofu, na kutoka moyoni. (Zaburi 62:8) Ndiyo, funzo la Biblia la kibinafsi na sala inayotoka moyoni ni mambo muhimu katika ibada yetu, nayo hutusaidia kuendelea kukaa katika upendo wa Mungu.

No comments:

Post a Comment

KAZI KUU TANO (5) ZA IMANI KATIKA MAOMBI.

Bwana YESU atukuzwe ndugu zangu. Karibu tujifunze Neno la MUNGU. Uhusiano ni upendo unaozaa ushirikiano na mawasiliano kati ya pande m...