Sunday, 17 September 2017

JITAHIDI KUPATA “UZIMA ULIO WA KWELI”

20, 21. “Uzima ulio wa kweli” ni nini, na kwa nini tumaini hilo ni zuri?
20 Yehova huwathawabisha watumishi wake waaminifu kwa kuwapa uzima, au uhai. Hata hivyo, ni uhai wa aina gani? Je, kweli uko hai sasa? Wengi wetu wangejibu, “Ndiyo.” Kwani, si tunapumua, tunakula, na kunywa? Bila shaka, tuko hai. Na tunapokuwa na furaha, huenda tukasema, “Haya ndiyo maisha!” Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba, katika maana halisi, hakuna mwanadamu yeyote ambaye ana uzima wa kweli.
Familia ikifurahia maisha katika paridiso duniani
Yehova angependa upate “uzima ulio wa kweli.” Je, utaupata?
21 Neno la Mungu linatuhimiza ‘tuushike imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Timotheo 6:19) Maneno hayo yanaonyesha kwamba tuna tumaini la kupata “uzima ulio wa kweli” wakati ujao. Ndiyo, tutakapokuwa wakamilifu, tutakuwa na uzima wa kweli, kwa maana tutaishi kama Mungu alivyokusudia tuishi. Tutakapoishi katika paradiso duniani tukiwa na afya kamili, amani, na furaha, ndipo tutakapofurahia “uzima ulio wa kweli”—uzima wa milele. (1 Timotheo 6:12) Je, hilo si tumaini zuri?
22. Unawezaje ‘kushika imara uzima ulio wa kweli’?
22 Tunawezaje ‘kushika imara uzima ulio wa kweli’? Akizungumzia jambo hilohilo, Paulo aliwahimiza Wakristo “wafanye mema” na “wawe matajiri katika matendo mazuri.” (1 Timotheo 6:18) Basi, ni wazi kwamba tunahitaji kutumia kweli ambazo tumejifunza katika Biblia. Lakini je, Paulo alimaanisha kwamba “uzima ulio wa kweli” ni malipo ya kutenda mema? Hapana, kwa maana tumaini hilo zuri hutegemea “fadhili zisizostahiliwa” kutoka kwa Mungu. (Waroma 5:15) Hata hivyo, Yehova anapenda kuwathawabisha wale wanaomtumikia kwa uaminifu. Angependa upate  “uzima ulio wa kweli.” Wale wanaokaa katika upendo wa Mungu ndio watakaopata uzima huo wa milele, wenye furaha na amani.
23. Kwa nini ni muhimu kukaa katika upendo wa Mungu?
23 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, ninamwabudu Mungu kupatana na maagizo yake yaliyo katika Biblia?’ Ikiwa tunafanya hivyo kila siku, basi tunatembea katika njia inayofaa. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ni kimbilio letu. Atawaokoa watu wake waaminifu katika siku hizi za mwisho zenye taabu za mfumo huu wa kale wa mambo. Pia, Yehova atatukomboa na kutuingiza katika mfumo mpya mtukufu ulio karibu. Tutakuwa na shangwe iliyoje kuishi wakati huo! Na tutakuwa na furaha iliyoje kwa kuwa tulifanya maamuzi yanayofaa katika siku hizi za mwisho! Ukifanya maamuzi yanayofaa sasa, utapata “uzima ulio wa kweli,” uzima ambao Yehova Mungu alikusudia, kwa umilele wote!

No comments:

Post a Comment

KAZI KUU TANO (5) ZA IMANI KATIKA MAOMBI.

Bwana YESU atukuzwe ndugu zangu. Karibu tujifunze Neno la MUNGU. Uhusiano ni upendo unaozaa ushirikiano na mawasiliano kati ya pande m...